Kitaifa
Kauli ya Serikali kuhusu vitambulisho vya Taifa

Dar es Salaam. Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Masauni amesema hadi Machi, 2024 kila Mtanzania atakuwa na kitambulisho cha Taifa.
Masauni amesema hayo leo Jumamosi Septemba 16, 2023 katika kijiji cha Nanguruwe akiwa katika ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye alisimama kuwasalimia wananchi katika moja ya kijiji mkoani Mtwara.
Masauni amesema Serikali imeshamlipa fedha mkandarasi anayetengeneza vitambulisho hivyo vinavyotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida).
“Katika bajeti iliyopita Serikali ilitenga Sh42.5 bilioni kwa ajili ya kutengeneza kadi milioni 11, fedha hizi zimeshalipwa kwa mkandarasi na anaendelea kuvitengeneza.
“Baadhi tumeanza kuzipokea tunatarajia vyote kuwa vimekamilika kabla ya Machi (mwaka 2024). Mwezi huu (Septemba) tumepokea kadi milioni mbili na tunaendelea kuzipokea kwa awamu kila mwezi hadi kufikia Machi mwakani hakutakuwa tena na ukosefu wa kadi za Nida kwa wananchi wote,” amesema Masauni.
Masauni ametumia fursa hiyo kuzitaka mamlaka mbalimbali za Serikali kuwahudumia wananchi wenye namba zilizotolewa na Nida wakati wakisubiri vitambulisho kwa kuwa tayari wanahesabika kuwa wana vitambulisho ila walipatiwa namba za vitambulisho vyao ili waweze kupata huduma mbalimbali ambazo hazitolewi bila mtu kuwa na namba au kitambulisho husika.
