Kimataifa

Sintofahamu Marekani, Trump apeleka Jeshi la Majini Los Angeles

Los Angeles, Marekani. Serikali ya Rais Trump imepeleka wanajeshi kati ya 500 na 700 wa Marekani katika Jiji la Los Angeles kusaidia wanajeshi wa Akiba wa Taifa pamoja na vyombo vya sheria vya eneo hilo, wakati maandamano dhidi ya ICE (Huduma ya Uhamiaji na Forodha) yalipogeuka kuwa ghasia katika jiji hilo mwishoni mwa wiki.

Kituo cha luninga cha CNN kimeripoti kuwa maofisa 500 kutoka Kikosi cha Mapambano ya Anga na Ardhi cha Marekani kilichopo California walihamishwa, wakati Shirika la Utangazaji la ABC News limeeleza kuwa maofisa 700 kutoka Kikosi cha Pili, Kundi la Saba la Wamarekani, kilichopo Twentynine Palms, California wamepelekwa katika jiji hilo.

Muda mfupi kabla ya taarifa za kupelekwa kwa maofisa hao kusambaa, leo Juni 10, 2025 Trump aliwaambia waandishi wa habari wa ABC kuwa,  “tutaona kinachotokea,” alipoulizwa kuhusu uwezekano wa kuwapeleka wanajeshi hao Los Angeles.

“Namaanisha, nafikiri tunasimamia hali hii vyema sana,” Trump alisema. “Nafikiri ingekuwa hali mbaya sana. Ilikuwa ikiendelea katika mwelekeo mbaya. Sasa inakwenda katika mwelekeo mzuri.”

Jumamosi, Trump alipeleka wanajeshi wa akiba ya Taifa mjini Los Angeles, hatua ambayo iliwakasirisha viongozi wa chama cha Democrat kama vile Gavana Gavin Newsom na Meya wa Los Angeles, Karen Bass.

Trump aliwalaumu Newsom na Bass kwa kuruhusu maandamano dhidi ya ICE ambayo yamegeuka kuwa ghasia, ambapo maofisa wa usalama wa serikali ya shirikisho, serikali za mikoa na za mitaa walishambuliwa na waandamanaji waliokuwa wakirusha mawe na kuwashambulia kwa vitu vya mlipuko.

Mtu mmoja aliiambia CNN kuwa maofisa hao wa jeshi wanatarajiwa kuchukua nafasi ya baadhi ya wanajeshi 2,000 wa akiba ya Taifa walioko katika mji huo kwa siku mbili sasa.

Miongoni mwa wanajeshi 2,000 wa akiba ya Taifa waliopo Los Angeles, takriban 300 pekee ndiyo waliokuwa wamewekwa katika mitaa. Kwa mujibu wa CNN, mawakili wa Wizara ya Ulinzi wanamalizia miongozo ya matumizi ya nguvu kwa maofisa hao.

Juzi Jumamosi Waziri wa Ulinzi, Pete Hegseth alisema kuwa, “wanajeshi wa kawaida wa Wamarekani walioko Camp Pendleton wapo tayari kwa hali yoyote ya tahadhari, iwapo ghasia zitazidi kuongezeka.”

Gavana Newsom ametaja maneno ya Hegseth kuwa  na tabia zisizo za kawaida. Newsom amesisitiza kuwa ghasia zimepigwa vita vya kutosha na mamlaka za majimbo na mitaa, lakini Rais Trump amesema kuwa mji ungeharibika kabisa kama asingechukua hatua. Trump pia amewaambia waandishi wa habari kuwa itakuwa vizuri iwapo mratibu wake wa mipaka, Tom Homan, atamkamata Newsom.

 

“Ametenda vibaya sana,” alisema rais kuhusu Newsom. “Tazama, nampenda Gavin Newsom, ni mtu mzuri, lakini hana ujuzi wa kutosha.”

Jimbo la California limefungua kesi dhidi ya serikali ya Trump kuhusu agizo la rais la kuwapeleka wanajeshi wa Akiba ya Taifa, likidai kuwa rais anajaribu kutengeneza machafuko na mzozo.

Katika kesi hiyo inadaiwa kuwa Trump aliwaita wanajeshi wa akiba kinyume cha katiba na kuvunja mamlaka ya Gavana wa Democrat, Gavin Newsom, bila kuwapo kwa tishio dhahiri la uvamizi au mapinduzi.

Newsom alisema kuwa hatua ya Trump inaandaa mazingira ya kutuma jeshi katika jimbo lolote iwapo atataka kufanya hivyo.

Telephone: +255 653 313 586 | Email: mhariri@chechetimes.com. | Address: 14216 Keko Magurumbasi